Tuesday 27 March 2012


 











NYAMA YA KUKU.

1.       Nina swala laniasi, nahitaji msaada,
Limekuwa si rahisi, kwangu imekuwa mada,
Sina hakika nahisi, jibu linanipa shida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

2.       Zinanitoka kamasi, nazidi poteza muda,
Naingiwa wasiwasi, kama nimepanda boda,
Swali limenisha kasi, nimekwama kama uda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

3.       Nilidhani filigisi, amenikanusha dada,
Kasema tamu kiasi, ina harufu ziada,
Shomboye kama girisi, mdomoni inakwida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


4.       Paja nikalinakisi, lapendwa hadi Finida,
Amenipinga Kaisi, amenicheka Sauda,
Eti mimi ndiyo basi, mbumbumbu au labda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

5.       Kuku anao ukwasi, vipande kwake ni ada,
Ukija kwa kinasisi, wa mitandao ya Voda,
Kidari chashika kasi, lakini si kwa Dauda,
Hasa ni kiungo gani kitamu nyama ya kuku.

6.       Kipapatio wadosi, wasema ndio waheda,
Kinaondoa mikosi, wakila na kuburuda,
Lakini kwa makasisi, hakimo kwenye jalada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


7        Amenambia Hamisi, kwa shingo ndio welda,
Akila anajihisi, ameshiba na faida,
Anavua na soksi, na kuimba dadadida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

8.       Makanyagio msosi, wameutaja makada,
Wanywaji kwa magrasi, acha nyinyi wanywa soda,
Kwamba kitu na boksi, kaone kwenye minada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


9        Ndugu zangu wa  Masasi, kabla kuvuka boda,
Ya kichwa wameasisi, wamesifu kina Sada,
Wasema yashinda ngisi, hata uile kwa dida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

10.     Hapa napiga krosi, nisimalize uroda,
Nawaacha waasisi, mnijaze ushuhuda,
Wajue kadamnasi, Kisiju hadi Singida,
Hasa ni kiungo gani , kitamu nyama ya kuku.







No comments:

Post a Comment