Friday 13 April 2012


USIRI WA FREEMASON NA MASHAKA YA JAMII


 Kwa kupindi kirefu wengi wetu tumekuwa tukisikia hadithi za kusisimua za Free Mason. Nasema za kusisimua kwa sababu zinasimulia mambo ya kutisha na ya ajabu ambayo yanaogopesha.

Binafsi sijampata mtu wa uhakika wa kunieleza vilivyo kuhusu kitu hiki Free Masom. Kiasi nashindwa kujua kama kundi hili ni la kidini, kichawi, kifisadi ama vipi. Nasema kundi hili linachanganya watu kwa sababu linasemekama lina mchanganyiko wa dini zote, makabila yote, jinsia zote isipokuwa kiuchumi, linachagua wenye mafanikio.

Kama kweli kundi hili si hatari kwa jamii, na kama kweli mambo yake ni mema ni kwanini halijiweki wazi. Usiri wa kundi hili unadhihirisha pengine kuna mambo ya aibu ambayo wanachama wake wanaogopa kama watajulikana  katika jamii itawaharibia  na kuwafanya wakimbiwe ama kuepukwa. Sijapata kumwona mtu hapa kwetu akijinadi kuwa yeye ni mwanachama hai wa kundi hilo. Kuna ubaya gani wa kujulikana kuwa mhusika. Mbona  wenye ukimwi wamejitokeza hadharani. Mbona walokole wanajinadi kila siku.  Kama hawaui, hawamwibii mtu na ni kundi la kusaidiana; wanapojifichaficha hawa wenzetu wanaogopa nini ? 

Hapo kipindi cha nyuma kidogo kulikuwa na afadhari; lakini sasa hivi  kumekuwa kila uchao kukitolewa orodha ya wanachama wa Free Mason wa kitanzania. Kwa jinsi orodha hiyo inavyopanuka kwa kasi nina hofu iko siku hata mimi mwenyewe nitasutwa na Ufree Mason. Sasa hivi kila mwenye mafanikio kifedha na madaraka anatajwa kuwa ni mwanachama wa Free Mason.

Nilidhani kwa nia njema wenzetu wa Free Mason wangelituweka sawa na kututoa wasiwasi kwa kutueleza bayana na waziwazi juu ya shughuli zao na majukumu yao au malengo yao ili kama kikundi kina neema basi wenye kuhitaji waingie. Haifurahishi kukaa kimya bila kusema chochote wakati jamii inawatuhumu kwa kila tukio baya hasa yahusuyo umwagaji damu. Sasa hivi basi likipata ajali na kuua watu kadhaa unaambiwa hiyo kazi ya Free Mason. Meli ikizama usemi ni uleule. Kifo cha kutatanisha cha mtu maarufu, madai hi hayohayo. Kwa hiyo jamii ielewe kuwa tuhuma hizo ni kweli ?

Thursday 12 April 2012




KIFO CHA KANUMBA

KULIA TU HAITOSHI BALI TUJIFUNZE KITU





 Tukumbuke daima kila limpatalo binadamu ni fundisho; fundisho kwake kama yu hai ama fundisho kwa waliobaki hai. Watu kumjadili marehemu Kanumba ama Lulu si kosa, ili mradi iwe ni kwa lengo la kujifunza. Wanapaswa waliobaki au tuliobaki tujue nini cha kupunguza ama nini cha kuongeza katika maisha yetu ili tupate ama yasitukute ya Lulu na Kanumba. Watu huhoji palipo na tukio lisilo la
kawaida na hukaa kimya pale penye tukio lililo la kawaida. Mijadala mingi imeshamiri kutokana na tukio zima la kifo cha Kanumba. Kifo cha Kanumba ni cha aina yake. Mahakama na ifanye kazi yake kwa uwezo wake, lakini na sisi tusizibane midomo katika kulitafakari tukio hili. Ebu fikiria, Lulu binti mdogo wa miaka 19 ak.a. 17 amekwenda kwa mpenzi wake a.k.a. mchumba wake a.k.a. msanii mwenzake. Huko nyumbani kumetokea majibizano a.k.a. ugomvi a.k.a msukumano. Lulu kuona Mpenzi a.k.a Mshkaji kadondoka anatoka na kuondoka; anaacha kisanga kwa ndugu yake. Hasubiri kujua hatma ya hali ya majeruhi ambaye ni kipenzi chake  kama ana hitaji msaada wa kukimbizwa hospitali ama huduma ya kwanza. Pengine alikuwa anawahi daladala, tax, ama anafuata gari aliloacha nje aje ambebe ama alikuwa ana kimbia so ama vyovyote vile. Laiti angelitulia na kuangua kilio pale penye tukio na kujutia mbele ya shemeji yake kwa kueleza ilivyokuwa n.k. maswali na udadisi wa akina yakhe usingelikuwa mkubwa. Yawezekana kwa udogo wa umri wake aliona hivyo ndivyo inafaa; lakini Lulu kama alivyokuwa marehemu Kanumba ni maarufu na watu wanamjua kwa kiasi kikubwa; hivyo wana nafasi ya kumweka katika fungu lolote wanaloona linafaa. Sasa wale wanaojifanya hawayaoni yote haya tuwaweke katika kundi gani....la waungwana, wastaarabu ama ndo walewale ? Pole sana Lulu na Mungu ailaze roho ya marehemu Kanumba mahali pema peponi.... Amen. Lakini ni ukweli usiopingika kuwa kifo hiki kimefundisha wengi mambo mengi.

Friday 30 March 2012


KAZI  USIYOITAKA UNAIOMBA YA NINI ?




Kutokana na hali ilivyokithiri imebidi niongelee hili pia kwani kwa hakika wengi wetu linatukera.

Jambo hili ni tabia ya baadhi ya watu ambao wamezagaa katika huduma mbalimbali lakini wana tabia chafu ambazo haziendani na  maadili ya huduma wanazozitoa.







Utamkuta mtu mwanamama au hata baba yuko hoteli kazi yake ni kuhudumia watu kuwasikiliza  waagizacho na kuwaletea wakitakacho lakini yeye daima ni kufanya ndivyo sivyo. Utamkuta sijui ni kwa sababu gani, lakini huwa hasikilizi maagizo hadi mwisho. Mtu ataagiza aletewe wali kwa nyama ya kuku, lakini yeye kama zuzu anamletea ugali kwa samaki. Anapolalamikiwa kuwa hivyo havikuagizwa, bila ya hata aibu huanza mabishano kwamba yeye ni mzoefu wa kazi yake na hawezi kukosea na maneno mengi ya kashfa kwa mteja.










Ama utamkuta dada yuko baa kazi yake kuuza bia. Mteja atafika kwenye baa hiyo, yeye hajali amezama anasoma gazeti la Ijumaa hujku akicheka pekeyake. Mteja akimstua ampe huduma huinuka huku akisonya na kwenda kuleta Kilimanjaro baridi kwa mteja bila ya hata kumuuliza na kumfungulia. Mteja akionyesha kushangaa, mhudumu huyu humbwatukia maneno na kusisitiza kuwa lazima alipie hicho kinywaji.





Ukienda hospitali nako kuna mengine. Watuwanakwenda na mgonjwa mahututi wanahangaika kumshusha kwenye gari, wahudumu na wamekaa wanaongelea kombe la UEFA. Ukiwauliza mbona hawachangamki, wanakujibu kuwa wao hawashughulikii  eneo hilo wasubiriwe wanaohusika. Wenye mgonjwa wakitaka kuchukua machela wambebe mgonjwa wao wanakuja juu na kuwambia hiyo machela ni ya chumba cha maiti wasiiguse. Watu hubaki wameduwaa hawaelewi wafanye nini; maana hawaelekezwi wafa kufahamishwa utaratibu ukoje.

Mambo haya ya huduma mbovu yamezagaa kila kona. Nenda Polisi, nenda mahakamani, nenda sokoni, madukani, mashuleni n.k. Watu wanafanya kazi kama wamelazimishwa. Wanafanya kazi kama wanajitolea kumbe wanalipwa kwa kazi hizo. Sasa jamani ni kwanini watu wanaomba kazi wasizozipenda na wasio na wito nazo ?

Raha Za Baikoko Tanga

Raha Za Baikoko Tanga

Wednesday 28 March 2012





GUBU LINAKERA KUPITILIZA




Katika mambo ambayo binadamu wengi hawawezi kuyavumilia; basi ni gubu.

Mtu mwenye gubu kwa kawaida huwa hana simile, hana subira, hana shukurani, hana huruma, na nadiriki kusema hata dini hana. Mtu mwenye gubu hajui kusamehe, hajui kusahau, hajui kubembeleza; yeye daima ni kulaumu, kulalamika, kusimanga, na kelele kibao. Naweza kusema ni heri ya mkorofi au mpigaji kuliko mwenye gubu.

Mwenye gubu hana dogo, mwenye gubu haridhiki mwenye gubu daima mdomo wake uko wazi unamwaga maneno kama bomba la maji nmachafu.

Mwenye gubu hudhani kuwa yeye ndiye anayejua, yeye ndiye anayeonewa, yeye ndiye mwangalifu; kwa ujumla mwenye gubu ni mbinafsi. Mwenye gubu hamwamini mwingine pamoja na kwamba yeye hujion ndiye anaaminika.

Kama hujawahi kuishi na mwenye gubu huwezi kuyajua haya, lakini kwa wale ambao wamepambana nao wanalijua hili; mwenye gubu ni moto wa kuotea mbali.

Lakini katika wenye gubu, wapo waliozaliwa na gubu hilo na wapo ambao wanatwezwa na mazingira au hali ya maisha kwa wakati ule. Pasmoja na tofauti zao hayuko mwenye nafuu.

Niseme tu kuwa gubu linakondesha haraka kushinda hata njaa.

Tuesday 27 March 2012


 











NYAMA YA KUKU.

1.       Nina swala laniasi, nahitaji msaada,
Limekuwa si rahisi, kwangu imekuwa mada,
Sina hakika nahisi, jibu linanipa shida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

2.       Zinanitoka kamasi, nazidi poteza muda,
Naingiwa wasiwasi, kama nimepanda boda,
Swali limenisha kasi, nimekwama kama uda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

3.       Nilidhani filigisi, amenikanusha dada,
Kasema tamu kiasi, ina harufu ziada,
Shomboye kama girisi, mdomoni inakwida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


4.       Paja nikalinakisi, lapendwa hadi Finida,
Amenipinga Kaisi, amenicheka Sauda,
Eti mimi ndiyo basi, mbumbumbu au labda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

5.       Kuku anao ukwasi, vipande kwake ni ada,
Ukija kwa kinasisi, wa mitandao ya Voda,
Kidari chashika kasi, lakini si kwa Dauda,
Hasa ni kiungo gani kitamu nyama ya kuku.

6.       Kipapatio wadosi, wasema ndio waheda,
Kinaondoa mikosi, wakila na kuburuda,
Lakini kwa makasisi, hakimo kwenye jalada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


7        Amenambia Hamisi, kwa shingo ndio welda,
Akila anajihisi, ameshiba na faida,
Anavua na soksi, na kuimba dadadida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

8.       Makanyagio msosi, wameutaja makada,
Wanywaji kwa magrasi, acha nyinyi wanywa soda,
Kwamba kitu na boksi, kaone kwenye minada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


9        Ndugu zangu wa  Masasi, kabla kuvuka boda,
Ya kichwa wameasisi, wamesifu kina Sada,
Wasema yashinda ngisi, hata uile kwa dida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

10.     Hapa napiga krosi, nisimalize uroda,
Nawaacha waasisi, mnijaze ushuhuda,
Wajue kadamnasi, Kisiju hadi Singida,
Hasa ni kiungo gani , kitamu nyama ya kuku.