Friday 30 March 2012


KAZI  USIYOITAKA UNAIOMBA YA NINI ?




Kutokana na hali ilivyokithiri imebidi niongelee hili pia kwani kwa hakika wengi wetu linatukera.

Jambo hili ni tabia ya baadhi ya watu ambao wamezagaa katika huduma mbalimbali lakini wana tabia chafu ambazo haziendani na  maadili ya huduma wanazozitoa.







Utamkuta mtu mwanamama au hata baba yuko hoteli kazi yake ni kuhudumia watu kuwasikiliza  waagizacho na kuwaletea wakitakacho lakini yeye daima ni kufanya ndivyo sivyo. Utamkuta sijui ni kwa sababu gani, lakini huwa hasikilizi maagizo hadi mwisho. Mtu ataagiza aletewe wali kwa nyama ya kuku, lakini yeye kama zuzu anamletea ugali kwa samaki. Anapolalamikiwa kuwa hivyo havikuagizwa, bila ya hata aibu huanza mabishano kwamba yeye ni mzoefu wa kazi yake na hawezi kukosea na maneno mengi ya kashfa kwa mteja.










Ama utamkuta dada yuko baa kazi yake kuuza bia. Mteja atafika kwenye baa hiyo, yeye hajali amezama anasoma gazeti la Ijumaa hujku akicheka pekeyake. Mteja akimstua ampe huduma huinuka huku akisonya na kwenda kuleta Kilimanjaro baridi kwa mteja bila ya hata kumuuliza na kumfungulia. Mteja akionyesha kushangaa, mhudumu huyu humbwatukia maneno na kusisitiza kuwa lazima alipie hicho kinywaji.





Ukienda hospitali nako kuna mengine. Watuwanakwenda na mgonjwa mahututi wanahangaika kumshusha kwenye gari, wahudumu na wamekaa wanaongelea kombe la UEFA. Ukiwauliza mbona hawachangamki, wanakujibu kuwa wao hawashughulikii  eneo hilo wasubiriwe wanaohusika. Wenye mgonjwa wakitaka kuchukua machela wambebe mgonjwa wao wanakuja juu na kuwambia hiyo machela ni ya chumba cha maiti wasiiguse. Watu hubaki wameduwaa hawaelewi wafanye nini; maana hawaelekezwi wafa kufahamishwa utaratibu ukoje.

Mambo haya ya huduma mbovu yamezagaa kila kona. Nenda Polisi, nenda mahakamani, nenda sokoni, madukani, mashuleni n.k. Watu wanafanya kazi kama wamelazimishwa. Wanafanya kazi kama wanajitolea kumbe wanalipwa kwa kazi hizo. Sasa jamani ni kwanini watu wanaomba kazi wasizozipenda na wasio na wito nazo ?

No comments:

Post a Comment