Friday, 30 March 2012


KAZI  USIYOITAKA UNAIOMBA YA NINI ?




Kutokana na hali ilivyokithiri imebidi niongelee hili pia kwani kwa hakika wengi wetu linatukera.

Jambo hili ni tabia ya baadhi ya watu ambao wamezagaa katika huduma mbalimbali lakini wana tabia chafu ambazo haziendani na  maadili ya huduma wanazozitoa.







Utamkuta mtu mwanamama au hata baba yuko hoteli kazi yake ni kuhudumia watu kuwasikiliza  waagizacho na kuwaletea wakitakacho lakini yeye daima ni kufanya ndivyo sivyo. Utamkuta sijui ni kwa sababu gani, lakini huwa hasikilizi maagizo hadi mwisho. Mtu ataagiza aletewe wali kwa nyama ya kuku, lakini yeye kama zuzu anamletea ugali kwa samaki. Anapolalamikiwa kuwa hivyo havikuagizwa, bila ya hata aibu huanza mabishano kwamba yeye ni mzoefu wa kazi yake na hawezi kukosea na maneno mengi ya kashfa kwa mteja.










Ama utamkuta dada yuko baa kazi yake kuuza bia. Mteja atafika kwenye baa hiyo, yeye hajali amezama anasoma gazeti la Ijumaa hujku akicheka pekeyake. Mteja akimstua ampe huduma huinuka huku akisonya na kwenda kuleta Kilimanjaro baridi kwa mteja bila ya hata kumuuliza na kumfungulia. Mteja akionyesha kushangaa, mhudumu huyu humbwatukia maneno na kusisitiza kuwa lazima alipie hicho kinywaji.





Ukienda hospitali nako kuna mengine. Watuwanakwenda na mgonjwa mahututi wanahangaika kumshusha kwenye gari, wahudumu na wamekaa wanaongelea kombe la UEFA. Ukiwauliza mbona hawachangamki, wanakujibu kuwa wao hawashughulikii  eneo hilo wasubiriwe wanaohusika. Wenye mgonjwa wakitaka kuchukua machela wambebe mgonjwa wao wanakuja juu na kuwambia hiyo machela ni ya chumba cha maiti wasiiguse. Watu hubaki wameduwaa hawaelewi wafanye nini; maana hawaelekezwi wafa kufahamishwa utaratibu ukoje.

Mambo haya ya huduma mbovu yamezagaa kila kona. Nenda Polisi, nenda mahakamani, nenda sokoni, madukani, mashuleni n.k. Watu wanafanya kazi kama wamelazimishwa. Wanafanya kazi kama wanajitolea kumbe wanalipwa kwa kazi hizo. Sasa jamani ni kwanini watu wanaomba kazi wasizozipenda na wasio na wito nazo ?

Raha Za Baikoko Tanga

Raha Za Baikoko Tanga

Wednesday, 28 March 2012





GUBU LINAKERA KUPITILIZA




Katika mambo ambayo binadamu wengi hawawezi kuyavumilia; basi ni gubu.

Mtu mwenye gubu kwa kawaida huwa hana simile, hana subira, hana shukurani, hana huruma, na nadiriki kusema hata dini hana. Mtu mwenye gubu hajui kusamehe, hajui kusahau, hajui kubembeleza; yeye daima ni kulaumu, kulalamika, kusimanga, na kelele kibao. Naweza kusema ni heri ya mkorofi au mpigaji kuliko mwenye gubu.

Mwenye gubu hana dogo, mwenye gubu haridhiki mwenye gubu daima mdomo wake uko wazi unamwaga maneno kama bomba la maji nmachafu.

Mwenye gubu hudhani kuwa yeye ndiye anayejua, yeye ndiye anayeonewa, yeye ndiye mwangalifu; kwa ujumla mwenye gubu ni mbinafsi. Mwenye gubu hamwamini mwingine pamoja na kwamba yeye hujion ndiye anaaminika.

Kama hujawahi kuishi na mwenye gubu huwezi kuyajua haya, lakini kwa wale ambao wamepambana nao wanalijua hili; mwenye gubu ni moto wa kuotea mbali.

Lakini katika wenye gubu, wapo waliozaliwa na gubu hilo na wapo ambao wanatwezwa na mazingira au hali ya maisha kwa wakati ule. Pasmoja na tofauti zao hayuko mwenye nafuu.

Niseme tu kuwa gubu linakondesha haraka kushinda hata njaa.

Tuesday, 27 March 2012


 











NYAMA YA KUKU.

1.       Nina swala laniasi, nahitaji msaada,
Limekuwa si rahisi, kwangu imekuwa mada,
Sina hakika nahisi, jibu linanipa shida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

2.       Zinanitoka kamasi, nazidi poteza muda,
Naingiwa wasiwasi, kama nimepanda boda,
Swali limenisha kasi, nimekwama kama uda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

3.       Nilidhani filigisi, amenikanusha dada,
Kasema tamu kiasi, ina harufu ziada,
Shomboye kama girisi, mdomoni inakwida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


4.       Paja nikalinakisi, lapendwa hadi Finida,
Amenipinga Kaisi, amenicheka Sauda,
Eti mimi ndiyo basi, mbumbumbu au labda,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

5.       Kuku anao ukwasi, vipande kwake ni ada,
Ukija kwa kinasisi, wa mitandao ya Voda,
Kidari chashika kasi, lakini si kwa Dauda,
Hasa ni kiungo gani kitamu nyama ya kuku.

6.       Kipapatio wadosi, wasema ndio waheda,
Kinaondoa mikosi, wakila na kuburuda,
Lakini kwa makasisi, hakimo kwenye jalada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


7        Amenambia Hamisi, kwa shingo ndio welda,
Akila anajihisi, ameshiba na faida,
Anavua na soksi, na kuimba dadadida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

8.       Makanyagio msosi, wameutaja makada,
Wanywaji kwa magrasi, acha nyinyi wanywa soda,
Kwamba kitu na boksi, kaone kwenye minada,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.


9        Ndugu zangu wa  Masasi, kabla kuvuka boda,
Ya kichwa wameasisi, wamesifu kina Sada,
Wasema yashinda ngisi, hata uile kwa dida,
Hasa ni kiungo gani, kitamu nyama ya kuku.

10.     Hapa napiga krosi, nisimalize uroda,
Nawaacha waasisi, mnijaze ushuhuda,
Wajue kadamnasi, Kisiju hadi Singida,
Hasa ni kiungo gani , kitamu nyama ya kuku.









VAZI LA TAIFA



Miongoni mwa mambo ambayo ni ya msingi kwa  Taifa letu na wananchi wake ni kuwa na utambulisho ambao utamfanya kila mwananchi wa  nchi hii atakapoonekana basi atambuliwe kuwa ni Mtanzania.

Miongoni mwa mambo hayo ni vazi la Taifa.

Kumekuwa na mawazo mengi juu ya vazi gain linalofaa kuwa vazi la  Taifa. Mimi nami kama Mtanzania sina budi kuchangia juu ya suala hili.

Nimekuwa nikiyaona mavazi mengi yanayopendekezwa kuwa mavazi ya Taifa. Tatizo nililogundua ni kuwa kwa kiasi Fulani tumekuwa nyuma kiubunifu kiasi kwamba mavazi au mitindo mingi inayoonyeshwa au kupendekezwa ni kama tunairudia au kuiiga toka kwa mataifa mengine.
 
Mimi kwa maoni yangu ningelipenda sisi tujikite katika rangi nne kwanza za taifa ambazo ni kijani; kwamba mtu awe huru kushona mtibndo wowote autakao, lakini pindi utakapokuwa umepangilia rangi zetu zote nne za taifa yaani kijani, njano, bluu na nyeusi basi vazi hilo liwe tayari ni la taifa.
 


Pendekezo langu la pili ni kutumia mavazi ya kimasai lakini katika rangi za taifa, basi hilo nalo liwe vazi la Taifa. Nasema hivi si kwamba ninadharau mavazi ya makabila mengine, lakini tutake tusitake, wamasai ndilo kabila pekee ambalo likekuwa na msimamo wa kulinda vazi lao kila waendako na kila waliko bila ya kuyumbishwa na mavazi haya ambayo yamekuwa yakiingia nchini mwetu kila siku. Hivyo Taifa kwa kuwaenzi, ichukue mavazi yao na kuyafanya ni ya Taifa.

 

 

MPENZI SHAIRI

  

Nilikuwa sijasema, siri ya moyoni mwangu,
Ila leo najituma, kutoa ukweli wangu,
Japo moyo waniuma, hiyo si hiari yangu,
Pokea ukweli wangu, Shairi ninakupenda.